As Salaam alaykum warahmatullah wabarakatuh. Karibuni sana marafiki waislamu tunufaike pamoja kwa kujifunza mas-ala mbalimbali kuhusu dini yetu.
Saturday, April 21, 2012
Mashitaka ya Jinai na utetezi
Na Dkt. Abdallah J. Saffari
Dibaji
KATIKA kitabu chake hiki, Bwana A. J. Saffari ameelezea kwa kirefu na kwa ufasaha hatua zinazohusu mashitaka na utetezi katika mashauri ya jinai kuanzia upelelezi, wajibu wa mpelelezi, na haki ya mshukiwa katika hatua hiyo. Pia ameelezea uendeshaji mashitaka yenyewe; vitu muhimu katika hati za mashitaka ya makosa mbalimbali, na utaratibu wote wa kuendesha mashitaka. Ushahidi, maana ya ushahidi, aina mbalimbali za ushahidi, na utaratibu mzima wa kutoa na misingi ya kutathmini ushahidi pamoja na masuala ya utetezi vimejadiliwa vizuri.
Kitabu hiki kinazungumzia pia wajibu wa mahakama katika hatua mbalimbali za usikilizaji wa haya mashauri ya jinai na misingi ya hukumu na adhabu inayotolewa mwishoni.
Kwa jumla, kitabu hiki ni cha manufaa kwa wale wote ambao kwa aina moja au nyingine wanahusika na suala zima la utoaji haki katika mashauri ya jinai. Kwani Bwana Saffari hakuorodhesha hatua na taratibu tu, bali amejaribu katika sehemu mbalimbali kuzungumzia chimbuko na misingi ya taratibu hizo na katika sehemu kadhaa ametoa maoni na mapendekezo yake. Inawezekana mtu asikubaliane naye katika sehemu kadhaa, lakini amejaribu kuangalia mambo aliyoyazungumzia kwa makini. Amefanya utafiti wa kutosha ili kutilia uzito mawazo aliyotoa.
Kwa kifupi hiki ni kitabu kinachofaa kusomwa na watu wote wenye hamu ya kujifunza au kuzidi kuendeleza majadiliano katika suala hili la haki na misingi inayoendelea kujengeka hapa kwetu nchini kuhusu utaratibu wa kutoa haki hasa katika mashauri ya jinai.
Jaji William K. Sekule.
Mashitaka ya Jinai na utetezi
Utangulizi
TAALUMA ya sheria imegawanyika katika matawi mawili makubwa: Madai na Jinai. Sheria za mikataba, ndoa, kazi na kadhalika ni mfano wa tawi la kwanza ambapo sheria zote ambazo zikikiukwa kosa hufanyika na adhabu hutolewa ni mfano wa lile tawi la pili. Aidha liko tawi jingine muhimu mno linaloelezea mwenendo yaani uendeshaji wa mashauri yote katika mahakama pamoja na kanuni za ushahidi. Kitabu hiki kinahusiana na tawi hili la mwisho.
Mwenendo wa mashitaka ya jinai ni utaratibu mzima wa upelelezi wa kosa, kushukiwa na kutiwa nguvuni kwa mtuhumiwa, kupekuliwa, kuandikisha maelezo, kufunguliwa mashitaka, kuwekwa mahabusu, kusikilizwa kwa shauri lenyewe, kuita mashahidi na kadhalika. Utetezi ni hatua inayofuatia mashitaka. Upande wa mashitaka unapomaliza kuita mashahidi wake mahakama huamua iwapo mshitakiwa, kwa ushahidi uliopo dhidi yake, anawajibika kujitetea.
Hivyo basi kujitetea, kama ilivyo kuendesha mashitaka, ni sehemu muhimu ya utekelezaji wa haki katika mashauri ya jinai. Muhimu vile vile ni uamuzi wa mahakama baada ya kuupokea na kuupembua ushahidi wa pande zote mbili.
Kwani huo ndio upeo wa shauri na sio siku zote mahakama huwa sahihi katika hukumu na adhabu inayotoa. Ndiyo maana kuna utaratibu wa rufani na masahihisho mahususi kwa kuangalia uhalali wa uamuzi wa mahakama ya daraja mbalimbali.
Kila mwanasheria, na hakika yeyote yule aliye na uzoefu wa mahakama, anaelewa kuwa mwenendo wa mashitaka ya jinai ni mithili ya mtambo unaoendesha chombo cha haki katika mashauri haya ya jinai yanayojadiliwa hapa. Kabla, na hata baada ya kukamatwa na kushtakiwa rasmi, kuna utaratibu ambao daima lazima ufuatwe kuhakikisha kuwa haki inatendeka hasa kutokana na dhana kwamba kila mtu hana hatia mpaka pale inapothibitishwa hivyo bila ya shaka yoyote ya maana.
Pamoja na mwenendo wa mashitaka ya jinai, kanuni za ushahidi ni muhimu kwa kiwango kile kile katika hatua mbili: Kabla ya wakati wa mashitaka. Kabla ya mashitaka kanuni za ushahidi ni zana muhimu ya kuamua iwapo kuna ushahidi wa kutosha dhidi ya mtuhumiwa kuweza kumfikisha mahakamani na wala sio kumshitaki tu na kumtesa. Wakati wa kusikiliza shauri lenyewe kanuni za ushahidi zinabainisha iwapo mshitakiwa ana hatia au la. Kwa bahati mbaya Sheria ya Ushahidi ni ngumu na inawatatiza hata baadhi ya wanasheria wa siku nyingi.
Hivyo basi azma ya kitabu hiki ni kumpa mwongozo kila mmoja mintaarafu ya utekelezaji haki katika mashitaka ya jinai. Kimekusudiwa kwa wanasheria na wasiokuwa wanasheria. Jitihada imefanywa kukiandika kwa wepesi bila ya kuzama katika tata za kitaaluma ambazo huweza kuwakanganya wasomaji wa kawaida. Lakini taratibu zote muhimu za kuandika kazi za kitaaluma, pamoja na tanbihi na istilahi za kutosha ziemzingatiwa hasa kwa faida ya watendaji katika mahakama na wanasheria.
Natumaini kuwa kitabu hiki kitaondoa dhana ya wale wenye taasubi ya Kiingereza kwamba sheria ni taaluma ambayo haieleweki wala kufundishika kwa Kiswahili ila Kiingereza pekee.
Upelelezi
MARA tu kunapotokea malalamiko ya kutendeka kwa kosa hatua ya kwanza muhimu ni kufanya upelelezi ili kupata ushahidi unaomhusisha mtu anayeshukiwa na kosa linalohusika. Upelelezi sio lazima uanze baada ya kupokea malalamiko ingawa hiyo ndiyo njia kuu ya kuanzisha upelelezi: yaani mtu anatendewa kosa na mtu anayemfahamu au asiyemfahamu na kwenda kituo cha usalama kutoa taarifa ya tukio hilo. Lakini, mathalan hata polisi wenyewe wanaweza kukuta mtoto mchanga ametupwa ndaniya pipa au mtu ameuawa na kutupwa kando ya barabara. Hiyo huwa namna ya pili ambayo husababisha upelelezi kufanyika.
Katika nchi nyingine upelelezi huweza kufanywa na mtu binafsi ambaye analalamika kutendwa kosa linalohusika au anaweza kumwajiri mtaalamu wa shughuli hiyo. Hali hiyo hufanyika zaidi kwa kuwa na imani kubwa juu ya uwezo wa mtaalam fulani kuliko kuliacha suala lote la upelelezi mikononi mwa polisi. Kinadharia, hapa Tanzania, mlalamikaji dhidi ya kosa la jinai hakatazwi kufanya upelelezi wake binafsi kumpata mhalifu. Lakini kwa kawaida kazi hiyo iko mikononi mwa Mkurugenzi wa Upelelezi wa Jinai kwenye Jeshi la Polisi.(Sheria ya Jeshi la Polisi, Sura ya 322)
Haikusudiwi kuingia katika mjadala wa mbinu zenyewe za upelelezi wa makosa ya jinai ambazo hutegemeana sana na aina ya makosa na mazingira yenyewe. Badala yake masuala muhimu kuambatana na hatua hii ya upelelezi yatajadiliwa. Nayo ni mtuhumiwa na mshitakiwa, hati ya kutia nguvuni, hati ya kupekuwa, hati ya kuita shaurini, maelezo ya mshitakiwa na mashahidi, pia dhamana.
Mtuhumiwa na Mshitakiwa
Mara nyingi upelelezi unapoanza huwa kuna mtu anayetuhumiwa kwamba ndiye aliyetenda kitendo kilichosababisha kosa linalohusika. Kunaweza kuwa na ushahidi wa mazingira au hata wa moja kwa moja kwamba mtu fulani ametenda kosa hilo. Mpelelezi anayehusika na kesi yenyewe hukusanya ushahidi wote huo na kutoa maoni yake kwa kiwango gani mshukiwa anahusika na ushahidi huo.
Iwapo ushahidi unaonekana kumwelemea na kumhusisha mtuhumiwa na kosa linalohusika basi hufunguliwa mashitaka naye huitwa mshitakiwa. Mashitaka huanza pale hati ya mashitaka dhidi ya mshitakiwa inapowasilishwa mahakamani.
Uamuzi sahihi wa kumfungulia mashitaka mtuhumiwa hutegemea sana kiwango cha uwezo wa anayechukua uamuzi huo katika kuupima ushahidi uliopatikana katika upelelezi dhidi ya mtuhumiwa. Kinadharia mtuhumiwa hufunguliwa mashitaka pale ambapo ushahidi wa kutosha umepatikana kiasi cha kuweza kufungua na kuendesha mashitaka dhidi yake kikamilifu. Lakini kwa bahati mbaya, kiutendaji, hivyo sivyo kama ambavyo itaonekana sura inayofuatia.
Hati ya kupekua
Ili kupata ushahidi dhidi ya mtuhumiwa mara nyingi inabidi apekuliwe mwenyewe au sehemu anamoishi. Kitendo cha kumpekua mtu huingilia uhuru na hata hadhi yake hivyo ni lazima kifanywe kwa mujibu wa masharti ya sheria.
Kuna namna mbili za kufanya upekuzi kwa njia ya halali. Kwanza ni kupata hati ya kupekua kutoka mahakama yoyote iliyo karibu na tukio lenyewe (F. 40, Sheria ya Mwenendo wa Jinai, Na. 1, 1985).
Pili kupata hati ya kupekua kutoka kwa Mkuu wa Kituo cha Polisi. Kwa kawaida hati hizi za njia ya pili hutolewa kwa Polisi. (F. 38, Sheria ya Mwenendo wa Jinai, i.h.j).
Hati ya kupekua inaweza ikatolewa na kutekelezwa siku yoyote ile hata Jumapili. (F. 40, Sheria ya Mwenendo wa Jinai, i.h.j). Kwa kawaida upekuzi hufanyika asubuhi hadi jioni lakini mahakama huweza kuamuru upekuzi ufanywe saa yoyote ile kama yanaona sawa kufanya hivyo.
Inatokea kuwa wakati wa kutaka kufanya upekuzi jengo au sehemu ya kupekuliwa imefungwa na mtuhumiwa hayupo. Ikiwa atakuwepo mtu mwingine yeyote anayeishi ndani ya jengo au sehemu hiyo au ana milki yake, mtu huyo atatakiwa kumpa polisi au yeyote mwenye hati hiyo, (baadaya kuonyeshwa), ruhusa na msaada wa kufanya upekuzi. (F. 43, Sheria ya Mwenendo wa Jinai, i.h.j).
Polisi au mtu mwenye hati ya upekuzi anaweza kutumia nguvu za kutosha kama vile kuvunja na kuingia au kutoka ndani ya jengo linalohusika kutekeleza amri hiyo. (F. 43 (2), Sheria ya Mwenendo wa Jinai, i.h.j).
Licha ya majengo, mtuhumiwa mwenyewe anaweza kupekuliwa. (F.42, Sheria ya Mwenendo wa Jinai, i.h.j). Iwapo mtuhumiwa ni mwanamke atapekuliwa na mwanamke mwenzake. Mwisho wa upekuzi hati itarejeshwa mahakamani ikionyesha kitu au vitu ambavyo vimepatikana. (F. 45(2), Sheria ya Mwenendo wa Jinai, i.h.j).
Vitu hivyo vilivyopatikana vitahifadhiwa hadi mwisho wa upelelezi au shauri lenyewe. Kama mtuhumiwa atashitakiwa na kupatikana na hatia kitu hicho (ambacho kitakuwa kielelezo) kitashughulikiwa kwa mujibu wa sheria. Na kama mshitakiwa amekata rufaa basi kitahifadhiwa hadi wakati wa kusikiliza rufani hiyo. Iwapo mshitakiwa amepelekwa Mahakama Kuu hicho kitahifadhiwa hadi wakati wa kusikilizwa shauri lake. (Hapa inahusiana na mashitaka ambayo husikilizwa na mahakama Kuu tu, kama vile kuzinga na maharimu, mauaji, uhaini na kadhalika).
Maelezo ya Mtuhumiwa, Mshitakiwa na Mashahidi
Mtuhumiwa, mshitakiwa na mashahidi wanaweza kutakiwa kutoa maelezo polisi ili kusaidia upelelezi na uendeshaji wa mashitaka. Utaratibu wa kuandika maelezo ya watu hao unatofautiana kama ambavyo itaelezwa hapa chini.
Tukianza na mashahidi ni kuwa polisi wana uwezo wa kumwita na kumhoji mtu yeyote ambaye wanaamini anaweza kutoa taarifa kusaidia upelelezi wa kesi inayohusika. (F.32. Sheria ya Jeshi la Polisi, i.h.j. Pia F.46 (1) Sheria ya Mwenendo wa Jinai, i.h.j).
Kama ni lazima maelezo ya mtu huyu yatanakiliwa na polisi. Maelezo hayo yanaweza baadaye kutumika katika kuendesha na kuthibitisha shitaka dhidi ya mshitakiwa. Kwa kawaida polisi huandika maelezo hayo wenyewe kadiri shahidi anavyoeleza. Mwisho humsomea Shahidi maelezo hayo na kumtaka afanye masahihisho yoyote kama yapo. Shahidi hutakiwa kuweka saini katika maelezo yake pamoja na saini ya mwandishi wa maelezo hayo. (F.48, Sheria ya Mwenendo wa Jinai, i.h.j).
Itabidi amfungulie mashitaka rasmi mtuhumiwa huyo halafu amhiarishe kama bado anapenda kutoa maelezo yake au la. (F.52(1), Sheria ya Mwenendo wa Jinai, i.h.j). Katika kufanya hivyo ni lazima mahakamani. (F.32(4), Sheria ya Mwenendo wa Jinai, i.h.j). Pia amueleze kuwa iwapo atakataa kumpa maelezo yoyote yanayoweza kuwa ushahidi kuhusiana na shitaka lenyewe atafikiriwa kuwa amefanya hivyo kwa nia ya kujiepusha na shitaka hilo. (F.52(4), Sheria ya Mwenendo wa Jinai, i.h.j).
Maana ya mashauri hayo dhidi ya mshitakiwa ni kujaribu kupata ushahidi muhimu kutoka kwake bila ya vipingamizi, lakini kwa hiari. Kwa kawaida polisi hawamuachii mshitakiwa atoe na kuandika maelezo yake mwenyewe bali humhoji na kuyaandika maelezo hayo. Askari wengine wanadai kuwa bila ya kumhoji mshitakiwa huwezi kupata ushahidi muhimu na wala huwezi kujua kama anasema kweli au anadanganya.
Utaratibu huu una tatizo moja kubwa katika utoaji haki kwa mujibu wa sheria. Ni hivi: polisi na upande wa mashitaka wanapoamua kuendesha kesi mahakamani huwa wanao ushahidi muhimu (kama mshitakiwa hakutoa maelezo ya uwongo) dhidi ya mshitakiwa. Lakini mshitakiwa huwa haelewi hali na uzito wa ushahidi wa upande wa mashitaka. Jambo hili lastahili kurekebishwa ili kumwezesha mshitakiwa aandae utetezi wake vizuri. Hivi sasa utaratibu huo unafanyika katika mashauri ambayo yanatanguliwa na Uchunguzi wa Awali kabla hayajasikilizwa na Mahakama Kuu.
Aidha, huweza kutumika katika mashauri ya madai. Pengine inasahauliwa kwamba baadhi ya mashauri katika mahakama ya wilaya ni magumu kisheria na kiushahidi kuliko hata yale yanayosikilizwa na Mahakama Kuu kwa mara ya kwanza. Na kwamba mashauri ya jinai huadhibiwa kwa kifungo au faini au vyote pamoja, hivyo kuna haja kubwa ya kumpa mshitakiwa kila nafasi ya kuandaa utetezi wake vizuri.
Hati ya kuitwa Shaurini
BAADA ya mashitaka kufunguliwa rasmi upande wa mashitaka hutoa majina ya mshitakiwa na mashahidi ambao unawahitaji katika uendeshaji wa kesi. Kufuatana na taarifa hiyo, mahakama huandika hati za kuwaita shaurini watu hao. Hivyo kuna hati za kuita shaurini washitakiwa na mashahidi.
Kila hati ya kuita mshitakiwa lazima iandikwe nakala mbili, itiwe saini na kugongwa mhuri na Hakimu au Afisa mwingine aliyepewa uwezo wa kufanya hivyo kama vile Msajili wa Mahakama na kadhalika. (F.100, Sheria ya Mwenendo wa Jinai, i.h.j). Hati hiyo itaandikwa na kupelekwa kwa mshitakiwa kumtaka ahudhurie mahakamani katika saa na siku iliyotajwa. (F.100(2), Sheria ya Mwenendo wa Jinai, i.h.j). Lazima pia ionyeshe kosa ambalo anakabaliwa nalo, pamoja na fungu la sheria linaohusu. (K.h.j.). Kwa mfano: Unatakiwa (mshitakiwa) kufika Mahakama ya Wilaya Kisutu saa tatu ya asubuhi Mei 10, 1995 kujibu shitaka la wizi dhidi ya fungu la 265 la Kanuni ya Adhabu, Sura ya 16 ya Sheria za Tanzania). Hati ya kumwita shahidi mahakamani itamtaka shahidi awasilishe mahakamani hati au vielelezo vyote alivyonavyo mntaarafu ya shauri linalohusika.
Polisi ndiyo hutumiwa kupeleka kwa wahusika hati za kuitwa shaurini. Lakini mtumishi yeyote wa umma au hata mtu yeyote tu yule anaweza kupeleka hati hiyo. Kila inapowezekana hati hiyo inatakiwa kuwasilishwa mikononi mwa mhusika mwenyewe kwa kumpa nakala moja ya hati yenyewe. (F.101(1),Sheria ya Mwenendo wa Jinai, i.h.j). Iwapo atatakiwa na mpelekaji wa hati hiyo, mhusika itabidi atie saini yake nyuma ya nakala ya pili ya hati hiyo kuthibitisha kuwa ameipokea. (F.1010(2), Sheria ya Mwenendo wa Jinai, i.h.j).
Kama mhusika hapatikani binafsi basi hati ya kumwita shaurini inaweza kuachwa kwa jamaa au mtumishi wake muradi awe mtu mzima. (F.102, Sheria ya Mwenendo wa Jinai, i.h.j). Na mtu huyo aliyeipokea hati hiyo kwa niaba ya mhusika atatia saini yake nyuma ya nakala ya pili ya hati hiyo iwapo atahitajika kufanya hivyo na mpelekaji. (K.h.j).
Na iwapo njia zote hizo zilizoelezwa hapo juu hazikuwezekana basi nakala moja ya hati ya kuita shaurini itaandikwa au kuwekwa katika sehemu ya nyumba yake ambapo mhusika ataiona kwa urahisi. (K.103, Sheria ya Mwenendo wa Jinai, i.h.j). Dhana ni kuwa mhusika atakuwa ameipata hati hiyo. Kama mhusika ni mtumishi wa serikali mahakama yatapeleka hati ya kuita shaurini kupitia kwa mkuu wake wa kazi. (K.h.j). Nakala mbili za hati hiyo zitapelekwa kwa mkuu huyo ambaye atawasilisha hati hiyo kwa mhusika na kumtaka atie saini yake nyuma ya nakala moja ya hati hiyo. Nakala yenye saini ya mhusika itarejeshwa katika mahakama iliyoitoa kama ushahidi kuwa imepokewa na mhusika.
Ikiwa kampuni au shirika linatakiwa kufika mahakamani hati ya kuita shaurini itapelekwa kwa njia ya rejesta kwa Katibu wa Kampuni au Shirika hilo au Afisa wake Mkuu. (F.105, Sheria ya Mwenendo wa Jinai, i.h.j).Dhana ni kuwa mawasiliano kwa njia ya Posta huwa kamili wakati barua imepostiwa.
Ikiwa kuna mabishano iwapo hati ya kuita shaurini imepokewa na mhusika au la, kiapo cha mpelekaji kuwa aliwasilisha hati hiyo kwa mhusika kwa namna inayotakiwa na sheria pamoja na nakala ya hati hiyo yenye saini ya mhusika vitakuwa ushahidi kuthibitisha uwasilishaji wa hati hiyo mpaka pale itakapothibitishwa vinginevyo. (F.108, Sheria ya Mwenendo wa Jinai, i.h.j).
Hati ya kutia Nguvuni
Isipokuwa kwa sababu zitakazoelezwa baadaye, mtu atatiwa nguvuni kutokana na hati rasmi ya kufanya hivyo.
Karibuni hati za kutia nguvuni zote hutolewa dhidi ya washitakiwa ambao wanashindwa kuhudhuria mahakamani katika siku na wakati ambao wametakiwa kufanya hivyo kwenye hati ya kuita shaurini.
Hati ya kutia nguvuni itatolewa na Katibu Kata, Katibu wa Baraza la Kijiji, Hakimu au Jaji baada ya kukubali maombi ya kiapo kutoka kwa mlalamikaji. (F.13(1), 110 NA 112(1), Sheria ya Mwenendo wa Jinai, i.h.j).Mara nyingi polisi, kwa niaba ya Jamhuri, ndiyo hufanya maombi hayo. Inasikitisha tu kuona kuwa aghalabu hawafanyi hivyo kwa kiapo. Hakimu anayetoa hati hiyo atatia saini yake pamoja na mhuri wa mahakama. (F.112(1) na 112(1), Sheria ya Mwenendo wa Jinai, i.h.j).
Kila hati ya kutia nguvuni lazima ieleze jina la mshitakiwa na shitaka ambalo anakabiliwa nalo. (F.112(2) Sheria ya Mwenendo wa Jinai, i.h.j). Aidha itaonyesha wazi majina ya watu ambao watatekeleza amri ya hati hiyo. Polisi ndiyo hupewa jukumu la kukamata washitakiwa. Lakini iwapo hapana budi mtu yeyote tu anaweza kutekeleza amri ya kumkamata mhusika. (F.114(1) Sheria ya Mwenendo wa Jinai, i.h.j).
Iwapo mshitakiwa anakabiliwa na shitaka ambalo si la mauaji au uhaini, mahakama yaweza kuamuru mshitakiwa huyo apewe dhamana kwa masharti ambayo mahakama yataeleza nyuma ya hati hiyo ya kutia nguvuni. (F.122(3), Sheria ya Mwenendo wa Jinai, i.h.j). Masharti hayo yataonyesha idadi ya wadhamini, kiasi cha fedha ambazo wao pamoja na mshitakiwa mwenyewe watatakiwa kutoa kama dhamana, na mwisho, saa ambayo watahitajika kufika mahakamani. (F.113, Sheria ya Mwenendo wa Jinai, i.h.j)..
Mshitakiwa ana haki na lazima aelezwe kwanza sababu za kukamatwa, (yaani kutiwa nguvuni). Kama mshitakiwa atasisitiza basi aonyeshwe hai yenyewe ya kumtia nguvuni. (F.117, Sheria ya Mwenendo wa Jinai, i.h.j).
Hata hivyo, polisi au raia anaweza kumtia nguvuni mtu bila ya hati ya kufanya hivyo kama mtu ameonekana akitenda kosa la jinai. Hii inatoa fursa ya kuzuia utendaji wa makosa ya jinai na kurahisisha upelelezi wake. Vinginevyo ni vigumu kumkuta mhalifu anasubiri akamatwe baada ya kutenda kosa.
Utiaji nguvuni, yaani ukamataji unafanyika kwa namna mbili kutegemea mazingira yenyewe. Moja ni kumkamata kabisa mhusika. ((F.11, Sheria ya Mwenendo wa Jinai, i.h.j). Wakati mwingine pingu hutumika kumfunga mtu anayekaidi kutiwa nguvuni. Njia nyingine ni ya matamshi kwamba mtu huyo amekamatwa rasmi na kuwa yuko chini ya ulinzi wa kisheria. (K.h.j). Amri kama hiyo ina uzito wa kisheria na ni kosa kutoitii. (F.22. Sheria ya Mwenendo wa Jinai, i.h.j). Njia hii ya pili ni ya kiungwana zaidi na hutumika mara nyingi isipokuwa kwa wale wakorofi tu. Mkamataji anaruhusiwa kutumia kiasi cha nguvu kinachotosha kumweka mkamatwaji chini ya ulinzi, na wala sio zaidi.
Nguvu inaweza kutumika dhidi ya mkamatwaji ikiwa ni lazima lakini kwa kila hali nguvu hizo zisikiuke kiwango kinachotosha kutekeleza ukamataji wenyewe. Kwa mfano jambazi laweza kupigwa kirungu ikiwa linakataa kutiwa mbingu, au linaweza hata kupigwa risasi ya miguuni kama linakimbia kutiwa nguvuni. Hata hivyo matumizi ya bunduki yanatakiwa kufanyika baada mkamataji kutoa onyo kwa mkamatwaji kuwa anakusudia kuitumia silaha hiyo kama hatasimama. Onyo sahihi zaidi ni kupiga hewani rasasi moja kabla ya kumlenga mkamatwaji.
Mkamatwaji anaweza kupekuliwa na vitu ambavyo vinashukiwa kuhusiana na uhalifu vinaweza kuchukuliwa na kuhifadhiwa kungojea kukamilika kwa upelelezi dhidi yake. (F.24(b), Sheria ya Mwenendo wa Jinai, i.h.j).Nguo alizovaa mkamatwaji hazitavuliwa. Ikiwa mkamatwaji atakutwa na silaha zozote za hatari zitachukuliwa na kuhifadhiwa mahakamani au kwenye kituo cha polisi. (F.27,Sheria ya Mwenendo wa Jinai, i.h.j)
Mtu anayekamatwa na polisi bila ya hati ya kufanya hivyo ni lazima afikishwe mahakamani, au kama amekamatwa na raia, afikishwe kituo cha polisi haraka iwezekanavyo katika muda usiozidi saa ishirini na nne. (F.30 na 32(1), Sheria ya Mwenendo wa Jinai, i.h.j). Kumuweka mkamatwaji chini ya ulinzi kwa muda mrefu bila ya kumfikisha mahakamani ni kosa. ( Dutto v. West Nile District Administration (1968) E.A..428).
Dhamana
Mtu aliye chini ya ulinzi wa kisheria anaweza akaweka na kupewa dhamana na kuachiwa huru hadi wakati wa siku ambayo atahitajika kufika sehemu anayotakiwa kama vile kituo cha polisi au mahakamani.
Dhamana huweza kuombwa na kutolewa katika hatua tatu tofauti: wakati wa upelelezi wa shauri (F.64(2), Sheria ya Mwenendo wa Jinai, i.h.j) usikilizaji wake (F.148, Sheria ya Mwenendo wa Jinai, i.h.j) na mwisho, kabla ya rufani kusikilizwa. (F.368, Sheria ya Mwenendo wa Jinai, i.h.j).
Wakati wa upelelezi wa kesi polisi wanaweza kumkamata yaani kumtia nguvuni mtuhumiwa ili awasaidie na upelelezi wa shauri linalohusika. Baada ya mahojiano wanaweza kumwachia mtuhumiwa huyo kwa dhamana. (F.64, Sheria ya Mwenendo wa Jinai, i.h.j). Hii hujulikana zaidi kama dhamana ya polisi. Dhamana haiwezi kutolewa iwapo mshitakiwa anashitakiwa kwa kosa la mauaji au uhaini. (F.148(5) Sheria ya Mwenendo wa Jinai, i.h.j). Hata hivyo baadhi ya mahakama duniani yamewahi kutoa dhamana katika kesi za mauaji licha ya sheria kukataza jambo hilo. Mathalan katika Owusu and Another v. The Public, (1980) GLR 469. Angalia pia Seida and Others v. The Ruplic (1978 1 GLR 67), Mahakama Kuu ya Ghana yalitoa dhamana kwa vile ilidhihirika kwamba shauri lenyewe lingechelewa mno kusikilizwa. Hadi wakati wa maombi ya dhamana, tayari mshitakiwa alikuwa amekaa rumande kwa zaidi ya miaka mitatu. Ilidhihirika pia kuwa hali yake ya afya ilizidi kuwa mbaya. Lakini sababu muhimu kupita zote ni kuwa mahakama yaliridhika kuwa hakukuwa na ushahidi unaotosheleza kufungua shitaka la mauaji ya kukusudia. Sababu kama hiyo pia ilitumiwa na Mahakama Kuu ya Tanzania kumpa dhamana mshitakiwa wa mauaji ya kukusudia katika R. v. Daimu Mkando na Wenzake (Maombi Maalum ya Jinai Na. 24, 1985, Mahakama Kuu, Arusha) na R. v. Patrick Soka na Wenzake( Uchunguzi wa Awali Na. 16, 1989, Mahakama Kuu, Arusha).
Licha ya makosa ya mauaji ya kukusudia dhamana pia haitatolewa iwapo mshitakiwa aliwahi kuvunja masharti ya dhamana au ameshitakiwa kwa kosa alilolitenda akiwa katika dhamana. Dhamana pia itakataliwa iwapo Mkurugenzi wa Mashitaka, atapinga kwa hati maalum kwamba dhamana isitolewe kwa vile itahatarisha usalama au manufaa ya taifa. (F.. 148(4) Sheria ya Mwenendo wa Jinai, i.h.j. Angalia pia F.35(2), Sheria ya Makosa ya Kiuchumi, Na. 13, 1984).
Katika Daud Pete v. R (Shauri Maalum la Jinai Na. 80, 1989, Mahakama Kuu, Mwanza) uwezo huu wa Mkurugenzi wa Mashitaka kupinga dhamana ulionekana kinyume cha Katiba ya Jamhuri ya Muungano ya Tanzania kwa vile unamnyima mshitakiwa haki yake ya kibinadamu ya kujitetea kabla hajakataliwa dhamana. Kwa bahati mbaya baadaye Mahakama ya Rufani ya Tanzania hayakulijadili suala hili kwa undani katikaR. v. Daudi Pete (Shauri la Jinai la Rufani Na. 28, 1990, Mahakama ya Rufani ya Tanzania) wakati ambapo Jamhuri ilipania kutengua hukumu ya awali ya Mahakama Kuu katika shauri hilo.
Mtuhumiwa alipofunguliwa mashitaka rasmi hatua nyingine huanza, ambayo inamkabidhi mikononi mwa mahakama kuanzia wakati huo mpaka shauri lake litakapomaliza kusikilizwa.
Dhamana huweza kutolewa kwa washitakiwa wa makosa yote isipokuwa yale yaliyotajwa punde tu. Vinginevyo mahakama bado yana uwezo wa mwisho kumwachia mshitakiwa kwa dhamana au la. Na vile mshitakiwa sio mhalifu hadi inapothibitishwa hivyo, dhamana hukataliwa pale tu kunapokuwa na sababu za msingi sana.
Masuala kadhaa hutiliwa maanani na mahakama yanapofikiria kukubali au kukataa ombi la dhamana. Uzito wa kosa ambalo mshitakiwa anakabiliwa nalo ni moja ya masuala hayo. Hofu ni kwamba iwapo mshitakiwa atapatikana na hatia anaweza kupewa adhabu kali, jambo ambalo huweza kumtisha au kumshawishi kutoroka akiwa nje ya dhamana.
Dhamana
Mtu aliye chini ya ulinzi wa kisheria anaweza akaweka na kupewa dhamana na kuachiwa huru hadi wakati wa siku ambayo atahitajika kufika sehemu anayotakiwa kama vile kituo cha polisi au mahakamani.
Dhamana huweza kuombwa na kutolewa katika hatua tatu tofauti: wakati wa upelelezi wa shauri (F.64(2), Sheria ya Mwenendo wa Jinai, i.h.j) usikilizaji wake (F.148, Sheria ya Mwenendo wa Jinai, i.h.j) na mwisho, kabla ya rufani kusikilizwa. (F.368, Sheria ya Mwenendo wa Jinai, i.h.j).
Wakati wa upelelezi wa kesi polisi wanaweza kumkamata yaani kumtia nguvuni mtuhumiwa ili awasaidie na upelelezi wa shauri linalohusika. Baada ya mahojiano wanaweza kumwachia mtuhumiwa huyo kwa dhamana. (F.64, Sheria ya Mwenendo wa Jinai, i.h.j). Hii hujulikana zaidi kama dhamana ya polisi. Dhamana haiwezi kutolewa iwapo mshitakiwa anashitakiwa kwa kosa la mauaji au uhaini. (F.148(5) Sheria ya Mwenendo wa Jinai, i.h.j). Hata hivyo baadhi ya mahakama duniani yamewahi kutoa dhamana katika kesi za mauaji licha ya sheria kukataza jambo hilo. Mathalan katika Owusu and Another v. The Public, (1980) GLR 469. Angalia pia Seida and Others v. The Ruplic (1978 1 GLR 67), Mahakama Kuu ya Ghana yalitoa dhamana kwa vile ilidhihirika kwamba shauri lenyewe lingechelewa mno kusikilizwa. Hadi wakati wa maombi ya dhamana, tayari mshitakiwa alikuwa amekaa rumande kwa zaidi ya miaka mitatu. Ilidhihirika pia kuwa hali yake ya afya ilizidi kuwa mbaya. Lakini sababu muhimu kupita zote ni kuwa mahakama yaliridhika kuwa hakukuwa na ushahidi unaotosheleza kufungua shitaka la mauaji ya kukusudia. Sababu kama hiyo pia ilitumiwa na Mahakama Kuu ya Tanzania kumpa dhamana mshitakiwa wa mauaji ya kukusudia katika R. v. Daimu Mkando na Wenzake (Maombi Maalum ya Jinai Na. 24, 1985, Mahakama Kuu, Arusha) na R. v. Patrick Soka na Wenzake( Uchunguzi wa Awali Na. 16, 1989, Mahakama Kuu, Arusha).
Licha ya makosa ya mauaji ya kukusudia dhamana pia haitatolewa iwapo mshitakiwa aliwahi kuvunja masharti ya dhamana au ameshitakiwa kwa kosa alilolitenda akiwa katika dhamana. Dhamana pia itakataliwa iwapo Mkurugenzi wa Mashitaka, atapinga kwa hati maalum kwamba dhamana isitolewe kwa vile itahatarisha usalama au manufaa ya taifa. (F.. 148(4) Sheria ya Mwenendo wa Jinai, i.h.j. Angalia pia F.35(2), Sheria ya Makosa ya Kiuchumi, Na. 13, 1984).
Katika Daud Pete v. R (Shauri Maalum la Jinai Na. 80, 1989, Mahakama Kuu, Mwanza) uwezo huu wa Mkurugenzi wa Mashitaka kupinga dhamana ulionekana kinyume cha Katiba ya Jamhuri ya Muungano ya Tanzania kwa vile unamnyima mshitakiwa haki yake ya kibinadamu ya kujitetea kabla hajakataliwa dhamana. Kwa bahati mbaya baadaye Mahakama ya Rufani ya Tanzania hayakulijadili suala hili kwa undani katikaR. v. Daudi Pete (Shauri la Jinai la Rufani Na. 28, 1990, Mahakama ya Rufani ya Tanzania) wakati ambapo Jamhuri ilipania kutengua hukumu ya awali ya Mahakama Kuu katika shauri hilo.
Mtuhumiwa alipofunguliwa mashitaka rasmi hatua nyingine huanza, ambayo inamkabidhi mikononi mwa mahakama kuanzia wakati huo mpaka shauri lake litakapomaliza kusikilizwa.
Dhamana huweza kutolewa kwa washitakiwa wa makosa yote isipokuwa yale yaliyotajwa punde tu. Vinginevyo mahakama bado yana uwezo wa mwisho kumwachia mshitakiwa kwa dhamana au la. Na vile mshitakiwa sio mhalifu hadi inapothibitishwa hivyo, dhamana hukataliwa pale tu kunapokuwa na sababu za msingi sana.
Masuala kadhaa hutiliwa maanani na mahakama yanapofikiria kukubali au kukataa ombi la dhamana. Uzito wa kosa ambalo mshitakiwa anakabiliwa nalo ni moja ya masuala hayo. Hofu ni kwamba iwapo mshitakiwa atapatikana na hatia anaweza kupewa adhabu kali, jambo ambalo huweza kumtisha au kumshawishi kutoroka akiwa nje ya dhamana.
Kwa hiyo mahakama huwa tayari kukubali dhamana kuhusiana na makosa madogo kuliko yale yenye adhabu kali kama vile kifungo cha muda mrefu. Katika shauri la Asoke v. R. (1971 H.C.D. n.192). Mrufani alipinga uamuzi wa Mahakama ya Wilaya kuyakataa maombi yake ya dhamana. Mrufani alikabiliwa na shitaka la wizi la shilingi milioni 250,000 mali ya serikali ya Tanzania. Alikuwa raia wa Kenya, Mkurugenzi wa Kampuni moja kubwa ya biashara Uganda, alikuwa na nyumba nzuri Uganda na Kenya. Ingawa alikuwa na wadhamini Watanzania wenye mali ya kutosha, Mahakama Kuu iliitupilia mbali rufani hiyo kwa sababu uwezekano wa kutoroka katika mazingira ya kesi hiyo usingefaa kupuuzwa.
Uwezekano wa kutenda kosa jingine au kulirudia lile lile pia hutiliwa maanani. Mifano ni mashauri haya mawili yafuatayo:
Katika kesi ya John Mswani na Wenzake v R. (1970 H.C.D. n.59) mrufani alipinga uamuzi wa mahakama ya awali kumkatalia dhamana. Alikuwa anakabiliwa na shitaka la wizi. Hata hivyo Jamhuri ilithibitisha kwamba wakati ambapo mrufani aliachiwa kwa dhamana mara ya kwanza alijihusisha na kosa jingine la kughushi hundi. Mahakama Kuu yaliridhika na maelezo hayo ya Jamhauri na kuikataa rufani ya John Mswani.
Katika kesi ya Jonathan Mwaniki v. R. (1970 H.C.D. n.177) Mahakama Kuu yalikataa rufani ya kupinga kukataliwa dhamana kwa vile mrufani alionekana anaweza kuendelea kujidai kwamba yeye ndiye aliyepewa shahada ya Juu kutoka Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kwa watu wengine (mbali ya mlalamikaji).
Kuvuruga amani na usalama wa jamii ni sababu nzuri ya kukataa dhamana iwapo itathibitisha hivyo. Kwa mfano katika kesi ya Mwita v. R. (1971 H.C.D. n.122). Mahakama Kuu yaliyakataa madai ya Jamhuri kupinga rufani kwa vile eti mrufani angepata nafasi ya kujilipiza kisasi dhidi ya mlalamikaji. Jamhuri haikutoa ushahidi kuthibitisha madai hayo ya kupinga dhamana. Aghalabu polisi hufanya hivyo kwa vile mashauri yao huyaanzisha kabla ya upelelezi kukamilika na ushahidi kamili kupatikana dhidi ya washitakiwa. Kwa bahati nzuri mahakama yanasisitiza kuwa hoja zote za kupinga maombi ya dhamana ziwe na ushahidi madhubuti au zitolewe kwa kiapo. Kwani endapo mahakama yatasikiliza na kuafikiana na madai, wasiwasi, na pengine hofu tu za waendesha mashitaka basi kutakuwa hakuna upeo wa madai hayo kiasi kwamba dhamana zitakataliwa kila wakati madai hayo yatakapotolewa.
Katika shauri la Bhangwanji Kakubhai v. R. ( T.L.R. 143) mrufani alipinga amri ya mahakama ya awali kumkatalia dhamana. Mrufani alikuwa ameshitakiwa kwa kosa la kuwa na dhahabu kinyume cha sheria. Upande wa mashitaka ulipinga dhamana kwa madai kuwa mshitakiwa alikuwa na nafasi na vielelezo ambavyo angeweza kuvitumia kuzuia kugunduliwa kwa biashara haramu ya dhahabu katika sehemu nyingine za Tanganyika. Yakikataa hoja hiyo Mahakama Kuu yalisema kwamba dai tu kuwa mrufani anazo habari na vielelezo ambavyo iwapo vitatumiwa vitavuruga upelelezi mzuri wa polisi ni la kinadharia mno, halieleweki na wala halitoshi kuwa sababu ya kumweka mrufani ndani wakati hakuna shaka yoyote kuwa atatoroka iwapo atapewa dhamana.
Mahakama hayo yalimaliza kwa kusema kwamba: "Sababu kuu ya kumtia mtu ndani ni kuhakikisha kuwa atahudhuria kusikiliza kesi dhidi yake. Sio sehemu ya sheria zetu kumweka mtu ndani kwa vile tu polisi hawapendi kuiona sura yake. (K.h.j). Hivyo kwa hakika hadi sasa suala kubwa kupita yote ambayo mahakama hujiuliza wakati wa kusikiliza maombi ya dhamana ni iwapo mwombaji atahudhuria kusikiliza shauri kila saa na siku mbele ya mahakama yanayohusika.
Masharti ya dhamana hutolewa na mahakama. Baadhi yake ni kuwa mshitakiwa aache hati ya kusafiria mikononi mwa polisi, kama anayo, pamoja na kuzuiliwa kutoka nje ya eneo maalum kama vile kijiji, mji na kadhalika. (F.148(6), Sheria ya Mwenendo wa Jinai, i.h.j). Mshitakiwa anaweza kupewa dhamana kwa uzito wa idadi ya wadhamini ambayo mahakama inaona inafaa.
Wadhamini hao wanatakiwa kuwa watu wenye kuaminika. Wanaweza kutakiwa walipe kiasi fulani mahakamani au watie saini mkataba wa kulipa kiasi fulani cha fedha iwapo mdhaminiwa atashindwa kufika mahakamani tarehe iliyopangwa. (F.151, Sheria ya Mwenendo wa Jinai, i.h.j). Au mshitakiwa anaweza kujidhamini mwenyewe kwa kutia saini mkataba wa kufika mahakamani siku inayotakiwa. (K.h.j).
Kiwango cha fedha za dhamana hutegemea mazingira ya shauri lenyewe lakini hakitakiwi kuwa kikubwa mno. (F.148(2), Sheria ya Mwenendo wa Jinai, i.h.j). Mahakama ya rufani yanaweza kupunguza kiwango cha fedha ambazo zimetakiwa kama dhamana au kubadilisha masharti mengine yoyote yaliyotolewa na mahakama ya awali kuhusiana na dhamana. (F.149, Sheria ya Mwenendo wa Jinai, i.h.j) Hii ina maana mshitakiwa anaweza kukata rufani ili apewe dhamana na Mahakama Kuu iwapo alinyimwa dhamana awali.
Mdhamini anaweza kujitoa kumdhamini mshitakiwa wakati wowote anapopenda kufanya hivyo mahakamani. Hali hiyo ikitokea mahakama yatamjulisha mshitakiwa atafute wadhamini wengine.
Mahakama ambayo awali yaliyakataa maombi ya dhamana yanaweza kuyakubali iwapo kutakuwa na sababu za maana za kufanya hivyo baadaye. Kwa mfano ikiwa upande wa mashitaka haupingi tena mshitakiwa hupewa dhamana, au pengine mshitakiwa ameweza kutimiza masharti ya dhamana yaliyomshinda awali kama vile kupata idadi ya wadhamini wanaoaminika au kima cha fedha kilichohitaijka. Na pengine dhamana hutolewa kwa vile sababu ambazo awali zilizuia dhamana kutolewa hazipo tena. Ikiwa mshitakiwa amewekwa ndani kwa kushindwa kutimiza masharti ya dhamana anaweza kuomba kupewa dhamana mara tu anapoweza kutimiza masharti hayo.
Kwa upande mwingine mahakama yanaweza kufuta dhamana yaliyompa mshitakiwa kama kuna sababu za maana za kufanya hivyo.
Mshitakiwa akitoroka mdhamini atafidia utoro huo kwa kulipa kiwango kilichokubaliwa na mahakama hapo awali. Dhamana kabla ya rufani zitajadiliwa katika matoleo yajayo.
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment